ZANZIBAR INA MWELEKEO MZURI WA KUIMARISHA AFYA

Na Khamis Haji, OMKR Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Mhe. Maalim Seif Sharif Hamad amesema mafanikio yaliyoweza kupatikana ...




Na Khamis Haji, OMKR
Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Mhe. Maalim Seif Sharif Hamad amesema mafanikio yaliyoweza kupatikana katika sekta ya afya miaka ya hivi karibuni ni ishara kuwa Zanzibar ina mwelekeo mzuri wa kuimarisha afya za wananchi na kukuza maendeleo yao. 
Maalim Seif amesema hayo (27 Novemba) wakati alipokuwa akifungua mkutano wa nane wa Tathmini ya Utekelezaji wa Mikakati ya Sekta ya Afya Zanzibar, unaofanyika hoteli ya Ocean View mtaa wa Kilimani mjini Zanzibar.
Amesema ni dhahiri hatua ya Zanzibar kuelekea kutokomeza maradhi ya Malaria, kupungua kwa asilimia kubwa vifo na matatizo yanayo wakumba akinamama wakati wa kujifungua na mengineyo, zimeibua matumaini makubwa kuimarika afya na maisha bora zaidi.
  
Aidha, Maalim Seif amesema mafanikio hayo yanaleta matumaini kuwa Zanzibar itamudu au kukaribia kabisa kutimiza malengo yaliyowekwa ya Milenia katika sekta ya Afya, ifikapo mwaka 2015.
Makamu wa Kwanza wa Rais alitoa mfano vifo vya akinamama wakati wa kujifungua mwaka 2008 vilikuwa 422 kati ya watu 100,000, lakini kutokana na juhudi kubwa zilizoweza kuchukuliwa vimeweza kupungua hadi kufikia 221 kati ya watu 100,000, punguo ambalo ni wastani wa asilimia 50.
Aliwapongeza watendaji na wataalamu wa Wizara ya Afya Zanzibar pamoja na washirika wa maendeleo kutokana na juhudi kubwa na moyo wa dhati wanao uonesha katika kufanikisha malengo ya Serikali ya kuimarisha afya bora za wananchi wa Unguja na Pemba.
Maalim Seif, hata hivyo alisema kwa upande wa maradhi ambayo hadi sasa yanaendelea kuwa changamoto kubwa, juhudi zaidi za kuwaelimisha wananchi namna ya kujikinga nayo ziendelezwe.
Ameahidi kwa upande wa Serikali itaendelea kuchukua juhudi kubwa zaidi katika kujenga mazingira yatakayoweza kupunguza kwa kiasi kikubwa changamoto hizo. Alisema juhudi hizo zinajumuisha kuwapatia wananchi huduma bora, ikiwemo maji safi na salama.
Amesema bado changamoto zipo katika baadhi ya maeneo, kama vile kudhibiti maradhi ya kichocho na Kifua Kikuu, ambayo pamoja na juhudi hizo kubwa zinazoendelea kuchukuliwa kote Zanzibar, bado hali sio ya kuridhisha. 
“Bado hatua za upimaji wananchi Kifua Kikuu hazitoshi, bado kuna changamoto ya wagonjwa kutomaliza dawa, maradhi ya kichocho pia ni tatizo, changmaoto hizi zinapaswa kushughulikiwa ipasavyo, ili tuweze kuondokana nazo”, alihimiza Maalim Seif.  
Waziri wa Afya, Mhe. Juma Duni Haji akizungumza katika mkutano huo alisema juhudi za kuelimisha wananchi njia bora kulinda afya zao na jamii kwa jumla zitaendelezwa, sambamba na kuhakikisha kunakuwepo wataalamu wa kutosha katika Sekta ya Afya Zanzibar.
Alizitaja miongoni mwa juhudi zinazochukuliwa kutatua changamoto ya uhaba wa wataalamu wa Kada hiyo, kuwa ni Serikali kusomesha wananchi katika vyuo vya ndani na nje ya nchi, juhudi ambazo zimeanza kuzaa matunda kutokana na kupatikanwa wahitimu ambao wanaendelea kutoa huduma Unguja na Pemba.
Amesema mwelekeo wa Wizara ni kuwahamaisha wananchi kujikinga zaidi na maradhi mbali mbali kuliko kusubiri kujitibu. “Tunahimiza Kukinga ni rahisi kuliko kutibu”, alisema Waziri Duni.
Akiwasilisha mada katika mkutano huo, Aisha A. Mohammed kutoka Wizara ya Afya Zanzibar, amesema mkazo zaidi uwekwe na Serikali pamoja na washirika wa Maendeleo katika kuhakikisha vifaa, wataalamu na mafunzo yanatolewa, ili kuhakikisha utoaji wa huduma za afya unazidi kuimarika.
Mkutano huo ambao hufanyika kila mwaka uliwashirikisha wadau mbali mbali, wakiwemo wataalamu wa Afya, Washirika wa Maendeleo, Wawakilishi kutoka Wizara ya Fedha, Jumuiya zisizokuwa za Kiserikali (NGOs) na baadhi ya watendaji kutoka taasisi nyengine za Serikali.
Credits: ZanziNews

Related

OTHER NEWS 5945171552441603273

FOLLOW US

.

LISTEN / DOWNLOAD MUSIC HERE:

Total Pageviews

RECENT

Archive

item