HIZI NDIZO MBINU MPYA ZA MAWASILIANO KUHUSU MAENEO YA KUUZA NA KUNUNUA MADAWA YA KULEVYA.

  LICHA ya vita dhidi ya dawa za kulevya nchini kupigiwa chapuo na wanasiasa, akiwamo Rais Jakaya Kikwete sambamba na kuwapo kwa Tume ya ...

LICHA ya vita dhidi ya dawa za kulevya nchini kupigiwa chapuo na wanasiasa, akiwamo Rais Jakaya Kikwete sambamba na kuwapo kwa Tume ya Kudhibiti Dawa za Kulevya, wauzaji na wateja wa biashara hiyo wamebuni mbinu mpya ya mawasiliano kuhusu maeneo ya kuuza na kununua dawa hizo, uchunguzi umebaini.
Uchunguzi huo wa muda mrefu i Jijini Dar es Salaam, na hususan maeneo ya Kinondoni na Magomeni umebaini kuwapo kwa ishara maalumu za kuwatambulisha wanunuzi wa dawa za kulevya kwamba sehemu fulani ndipo dawa hizo huuzwa.
Kwa mujibu wa uchunguzi huo, kila unapoona jozi ya viatu imetundikwa katika nyaya za umeme barabarani basi, mita chache tu kuna biashara ya kuuza na kununua dawa za kulevya kwa kuzingatia mahitaji yako. 

Mwandishi wetu amefika katika baadhi ya maeneo hayo na kununua baadhi ya dawa hizo ikiwa ni sehemu ya kuhakiki uchunguzi wetu kwa mujibu wa matakwa ya kitaaluma na kujiridhisha kwa namna gani vyombo husika, licha ya kuwapo kwa sheria za kupinga biashara hiyo, vimekuwa vikizidiwa maarifa.
Kuning’iniza jozi za viatu
Uchunguzi wa Raia Mwema, umebaini kuwa mtandao wa wauzaji dawa za kulevya ambao ndio wauzaji wadogo wadogo wamekuwa wakitambuana kwa jina maalumu la “mapusha” na kwamba vijana hao ni miongoni mwa wakazi wa maeneo husika na wengine wakiheshimika katika mitaa wanayoishi.
Lakini licha ya kuwa na jina maalumu la kimtandao, wahusika hao wamekuwa wakitumia mbinu hiyo ya kutundika jozi ya viatu katika nyaya za umeme kama zinavyoonekana katika picha iliyopigwa na timu ya waandishi wetu iliyohusika na uchunguzi wetu.
Ni aina maalumu ya viatu
Si kila aina ya viatu inaweza kutundikwa kama utambulisho wa kuwapo kwa “maduka” ya dawa za kulevya katika maeneo husika.
Aina hiyo maalumu ya viatu inaitwa “All Star”. Ni viatu vilivyoko katika muundo maalumu mithili ya “buti”. Katika baadhi ya maeneo, timu ya waandishi wetu ikielekezwa na ishara hizo za viatu imefika na kununua dawa hizo.
Uchunguzi wetu umebaini kuwa katika Wilaya ya Kinondoni, Dar es Salaam mbinu hiyo ya kuning’iniza jozi ya viatu imekuwa ikitumiwa mno katika maeneo ya Tandale, Kinondoni-Mkwajuni, Msasani, Kinondoni B katika mitaa ya Wibu, Togo na Ufipa jirani na Makao Makuu ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA).
Ana kwa ana na watumiaji ‘unga’
Katika vijiwe hivyo, mwandishi wetu akiigiza kama mmoja wa watumiaji sugu wa dawa hizo haramu za kulevya, alipenya na kuzungumza na baadhi ya watumiaji halisi wa dawa hizo.
Mmoja wa watumiaji hao aliyekutana na mwandishi wetu katika ‘kijiwe’ cha Mtaa wa Wibu, Kinondoni ambaye baada ya mazungumzo ‘kukolea’ kati yake na mwandishi wetu, ilibidi mwandishi ajitambulishe rasmi, alikiri kuwa katika kila eneo zinapouzwa dawa hizo viatu vimekuwa vikining’inizwa juu ya nyaya za umeme.
Mtumiaji huyo wa dawa za kulevya ambaye katika habari hii hatutataja jina lake, alimweleza mwandishi wetu; “Sina uhakika sana na mbinu hiyo ya kutundika ‘All Star’ (jozi za viatu) juu ya nyaya za umeme kuwa ni alama ya kuuzwa mdude (dawa za kulevya), lakini naweza kukubaliana na maneno yako kwani maeneo yote kunakouzwa ‘mdude huwaga’ nakuta alama hiyo.
“Zamani tulikuwa tunaiga Wamarekani kutundika ‘All Star’ katika nyaya za umeme, kwa sasa hata sijui kuna uhusiano gani na biashara hii. Ila naweza kukuthibitishia kuwa ni kweli kila kunapouzwa ‘mdude’ huwa kuna viatu aina ile vinaning’inia kwenye nyaya.”
Mwandishi wetu pia alizungumza na kijana mwingine ambaye naye ni muuzaji mdogo wa dawa hizo na hapa, kwa sababu maalumu tutamwita jina lisilo halisi la Kijiko Issa.
Mwandishi wetu alikutana na kijana huyo anayeishi mtaa wa Togo, Kinondoni B jijini Dar es Salaam. 
Kijiko alitambulishwa kwa mwandishi wetu na Baraka kuwa yeye ndiye pusha (muuzaji) wa dawa za kulevya. Pusha (muuzaji) huyo katika mazungumzo yake na mwandishi wetu, hakuwa tayari kuthibitisha kuwa utundikaji jozi za viatu katika nyaya za umeme ni ishara ya kuuza ‘unga’ eneo hilo.
Lakini baada ya mazungumzo marefu na mwandishi wetu, Kijiko alisema; “Mimi naona tu maeneo mengi ninapokwenda kununua ‘busta’ (kifuko cha dawa za kulevya chenye uwezo wa kuzalisha kete 200 mpaka 250), huwa nakuta ‘All Star’ zimetundikwa juu ya umeme lakini kiukweli sijui maana yake nini.
“Kwa mfano mtaa wa Ufipa karibu na ofisi za CHADEMA kuna dogo ‘anabana mzigo’ (anauza dawa) pale au ukienda Bonde la Mkwajuni pembeni ya barabara utakuta viatu vingi vipo juu ya umeme pale pia kuna jamaa wanabana mzigo.”
Maelezo ya mamlaka ya udhibiti
Timu yetu haikuishia hapo bali ilikwenda katika ofisi za Kikosi cha Kupambana na Dawa za Kulevya nchini na kukutana na Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi, ambaye ni mkuu wa kitengo cha kudhibiti dawa za kulevya nchini, Godfrey Nzowa.
Kamanda Nzowa alimweleza mwandishi wetu kuwa, anazo taarifa za kila mbinu mpya inayotumiwa na wauzaji wakubwa na wadogo wa dawa za kulevya nchini.
Kwa mujibu wa Kamanda Nzowa, wanayo timu maalumu ya askari katika kila eneo linalosifika kwa biashara hiyo.
“Hiyo mbinu nimeisikia kutoka kwa vijana (askari) wangu, lakini nasi pia hatuna uhakika nayo kwani bado ni mpya ila tunashukuru kwa utafiti wenu nasi tutaufanyia kazi utafiti huo,” alisema Nzowa.
Sheria inalenga vigogo wa ‘unga’
Hata hivyo, katika maelezo yake, Kamanda Nzowa alisema ingawa kikosi chake kinashiriki kikamilifu kudhibiti kila kundi la wauzaji wa dawa hizo, sheria inalenga zaidi kudhibiti waingizaji wa dawa hizo nchini kuliko wasambazaji.
“Sisi tunafuata sheria ya kudhibiti dawa za kulevya sura ya 95 (The drugs and prevention of illicit traffic in drugs) ambayo inaegemea sana katika waingizaji kuliko watumiaji na wasambazaji, ingawa upande huo nao hatuufumbii macho,” alisema Kamanda Nzowa.
Kilo moja huathiri watu milioni moja
Lakini Kamanda Nzowa alizungumzia pia kiwango cha madhara, yaani kwa namna gani kiwango kidogo tu cha dawa za kulevya kinavyokuwa na uwezo wa kuathiri idadi kubwa ya watumiaji.
Akifafanua Kamanda Nzowa, alisema mtumiaji huweza kutumia kiwango cha kati ya gramu 0.01 na 0.11 ambayo ni kete moja na kwamba, kilo moja ya dawa za kulevya huweza kuathiri takriban watu (watumiaji) milioni moja.
Alisema ingawa lengo la kikosi chake ni kuangamiza matumizi ya dawa za kulevya nchini lakini changamoto katika kufikia mafanikio ni nyingi na zimekuwa zikiongezeka kila siku.
Alizitaja baadhi ya changamoto hizo kuwa ni pamoja na kukosa bajeti ya kutosha kutoka serikalini. Lakini wakati bajeti ikiwa ndogo, vigogo wauza dawa za kulevya wamekuwa na uwezo mkubwa kifedha. via JF

Related

TUJUZANE 8028362460765492916

FOLLOW US

.

LISTEN / DOWNLOAD MUSIC HERE:

Total Pageviews

item