ZANZIBAR YATIA SAINI NA KAMPUNI YA SHELL KATIKA KUSHIRIKI KUENDELEZA SEKTA YA MAFUTA NA GESI

Na Said Ameir, Uholanzi Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Kampuni ya Mafuta ya Shell ya Uholanzi zimetia saini Makubaliano ya Ushir...

Na Said Ameir, Uholanzi
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Kampuni ya Mafuta ya Shell ya Uholanzi zimetia saini Makubaliano ya Ushirikiano katika kuendeleza sekta ya mafuta na gesi.
Makubaliano hayo yametiwa saini juzi tarehe 28 Agosti, 2013 mjini The Hague ambapo Waziri wa Ardhi, Makazi, Maji na Nishati Ramadhani Abdalla Shaaban alitia saini makubaliano hayo kwa niaba ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar na Mwakilishi wa Kampuni Shell Tanzania Axel Knospe alitia saini kwa niaba ya  Kampuni hiyo.
Makubaliano hayo yamefikiwa mjini The Hague wakati wa ziara ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed inayoendelea nchini humo.
Kabla ya kusainiwa kwa makubaliano hayo Dk. Shein alifanya mazungumzo na Uongozi wa juu wa kampuni ya Shell  yaliyojielekeza katika kuimarisha ushirikiano kati ya Serikali ya Zanzibar na Kampuni hiyo.
Kwa mujibu wa makubaliano hayo Kampuni ya Shell itaisaidia Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kujenga uwezo wa kitaalamu, katika hatua za awali za uendelezaji wa sekta hiyo.
 Sambamba na hatua hiyo Kampuni ya Shell itasaidia pia shughuli za maendeleo ya vijana katika kuwajengea uwezo kwa kuwapatia elimu na mafunzo mbalimbali yakiwemo ya stadi za ujasiriamali.
 
  Akizungumza mara baada ya kutia saini makubaliano hayo Waziri wa Ardhi, Makazi, Maji na Nishati Ramadhani Abdalla Shaaban alisema “kutiwa saini kwa makubaliano hayo ni hatua moja kubwa na mwelekeo sahihi katika jitihada za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuendeleza sekta ya nishati Zanzibar”
Kwa upande wake Mwakilishi wa Kampuni ya Shell Tanzania Bwana Axel Knospe alieleza kuwa wakati mashauriano yakiendelea kati ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na ile ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania juu ya kuliondoa suala la mafuta na gesi katika mambo ya muungano, Kampuni hiyo itaendelea na dhamira yake ya ushirikiano na Zanzibar hadi hapo muda utakapokuwa tayari kuanza kazi ya shughuli za uchimbaji mafuta na gesi ambapo itaifanya kazi hiyo kwa kuzingatia uwajibikaji kiuchumi, kijamii, kimazingira na  kuifanya sekta hiyo kuwa endelevu
“wakati Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania zikishughulikia kwa pamoja suala la kisheria na kisera kuipatia Zanzibar haki pekee ya kuendeleza sekta ya mafuta na gesi Zanzibar, Kampuni ya Shell itaendelea na dhamira yake ya kushirikiana na Zanzibar hadi hapo muda muafaka utakapofika kuanza shughuli za uchimbaji wa mafuta na gesi” alieleza bwana Axel Knospe.
Wakati akizungumza na Rais wa Zanzibar mjini hapa juzi Waziri wa Biashara ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa wa Uholanzi Bibi Lilianne Ploumen alimueleza Rais kuwa Serikali ya nchi hiyo iko tayari kutumia utaalamu na uzoefu wake katika sekta ya mafuta na gesi kuisaidia Zanzibar kuendeleza sekta hiyo.
Bibi Ploumen alieleza kuwa Serikali ya nchi hiyo iko tayari kutoa fursa za mafunzo kwa watumishi wa Serikali ya Zanzibar katika sekta ya nishati ili kuhakikisha kuwa wanakuwa na uzoefu katika kusimamia rasilimali hizo, utunzaji wa mazingira na ushiriki wa wananchi katika matumizi ya rasilimali hiyo kuepusha migogoro.
“Mambo ya msingi ya kupewa kipaumbele ni pamoja na namna ya uendeshaji, usimamizi na matumizi bora ya rasilimali hizo, ushirikishwaji wananchi na utunzaji mazingira”alieleza bibi Ploumen na kusisitiza haja ya Zanzibar kujifunza kutoka nchi nyingine kuepuka makosa yaliyofanywa na baadhi ya nchi ikiwemo Uholanzi yenyewe.
Dr. Shein anamaliza  ziara yake ya siku tano nchini Uholanzi leo  na anatajiwa kurejea nyumbani Jumapili ijayo.
Katika ziara hiyo Dk Shein amefuatana na Waziri wa Ardhi, Makazi, Maji na Nishati wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Ramadhani Abdalla Shaaban, Waziri wa Miundombinu na Mawasiliano Rashid Seif Suleiman, Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa Mahadhi Juma Maalim na Mshauri wa Rais Ushirikiano wa Kimataifa, Uwekezaji na Uchumi, Balozi Mohamed Ramia.

Related

OTHER NEWS 4458839714152637810

FOLLOW US

.

LISTEN / DOWNLOAD MUSIC HERE:

Total Pageviews

RECENT

Archive

item