BALOZI WA KUDUMU WA UMOJA WA MATAIFA AUGUSTINE MAIGA AKUTANA NA RAIS DK.SHEIN

  Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein akibadilishana mawazo na Balozi wa kudumu wa Umoja wa Mat...

 Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein akibadilishana mawazo na Balozi wa kudumu wa Umoja wa Mataifa (Mstaafu) wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, New York, Marekani Mhe. Augustine Maiga alipofika Ikulu Mjini Unguja leo.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein akibadilishana mawazo na Balozi wa kudumu wa Umojawa Mataifa(mstaafu) wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, New York, Marekani Mhe. Augustine Maiga alipofika Ikulu Mjini Unguja leo ( Picha na Ikulu Zanzibar)


STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
 
 
  Zanzibar                                                                                                                        19.11.2014
 
MAFANIKIO yaliofikiwa katika uimarishaji wa miradi ya maendeleo hapa Zanzibar sambamba na vivutio vyake vya utalii yote kwa pamoja yameweza kuijengea sifa kubwa Zanzibar Kimataifa.
Balozi wa Kudumu wa Umoja wa Mataifa (Mstaafu) wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Augustine Maiga aliyasema hayo leo wakati alipokuwa na mazungumzo na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein Ikulu mjini Zanzibar.
Katika maelezo yake Balozi Maiga, alimueleza Dk. Shein kuwa jina la Zanzibar limekuwa ni kigezo kikubwa cha mafanikio yaliopatikana katika miradi yake ya maendeleo ikiwemo kupambana na Malaria, kupunguza vifo vya akina mama na watoto, elimu, maambukizo ya virusi vya Ukimwi pamoja na sekta nyengine za kimaendeleo.
Akitolea mfano mafanikio yaliopatikana katika kupambana na Malaria, Balozi Maiga alisema kuwa Zanzibar imeweza kupata mafanikio makubwa ambayo ni ya kuigwa kwa nchi nyengine duniani hatua ambayo Umoja wa Mataifa nao unajivunia kwa hilo hasa katika kufikia Malengo ya Milenia.
Aidha, Balozi Maiga alimueleza Dk. Shein kuwa utalii wa Zanzibar umeweza kuwa ni kivutio kikubwa duniani hatua ambayo imepelekea watalii wengi kuwa na hamu ya kuja kuitembelea Zanzibar kutokana na vivutio vyake zikiwemo fukwe pamoja na sehemu zake za kihistoria.
Balozi Maiga pia, alitoa pongezi ambazo zimekuwa zikitolewa na viongozi wa Umoja wa Mataifa mara kwa mara kwa Zanzibar kutokana na kufanikiwa kuwepo kwa pamoja mashirikika ya Umoja wa Mataifa ‘ONE UN’ hapo katika Jengo la ZSTC Kinazini hali ambayo imeweza kuleta ufanisi mkubwa wa kikazi kwa mashirikika hayo hatua ambayo imeweza kuigwa na nchi nyengine duniani kama vile Vietnam.
Akimueleza Rais juu ya juhudi mbali mbali alizozichukua katika utendaji wake wa kazi akiwa New York, Marekani pamoja na wakati alipokuwa nchini Somali katika mikakati ya kusaka amani ya nchi hiyo, Balozi Maiga alisema kuwa Muungano wa Tanganyika na Zanzibar umewavutia nchi kadhaa ambazo wako tayari kuja kujifunza kutokana na mafanikio yake.
Pamoja na hayo, Balozi Maiga alimueleza Dk. Shein kuwa Tanzania imeweza kupata pongezi kubwa na kuweza kujijengea sifa kubwa ndani ya Umoja wa Mataifa kwa harakati zake za kuunga mkono harakati za kusimamia amani katika ndani na nje ya bara la Afrika.
Balozi Maiga aliongeza kuwa kumeshajitokeza Makampuni kadhaa ambayo yana nia ya kuunga mkono sekta ya elimu kwa lengo la kuanzisha Mradi wa Maktaba kwa kuanzisha maktaba kwa ajili ya kuwasaida wanafunzi pamoja  na wanajamii sambamba na kuwajengea uwezo vijana kujifunza masomo ya kompyuta kwa kushirikiana na Wizara husika ambapo kati ya maeneo sita ya Tanzania yatakayojengwa maktaba hizo, Zanzibar nayo imepata fursa hiyo.
Nae Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein alitoa pongezi zake kwa Balozi huyo wa Kudumu wa Umoja wa Mataifa (Mstaafu) wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuitumikia vyema nchi yake katika kipindi chake chote alichofanyakazi ndani ya umoja huo.
Dk. Shein alisema kuwa Zanzibar imeweza kujijengea sifa kubwa Kimataifa kutokana na mashirikiano mazuri inayopata sambamba na juhudi za makusudi inazozichukua katika kuimarisha miradi yake ya maendeleo ili kufikia lengo lililokusudiwa.
Alieleza kuwa mafanikio yaliopatikana katika kupambana na Malaria pamoja na kupambana na maambukizo ya virusi vya Ukimwi na kupunguza vifo vya akina mama wajawazito yameweza kuijengea jina Kimataifa huku akisisitiza kuwa juhudi zitaendelea kuchukuliwa na Serikali anayoiongoza.
Kwa upande wa sekta ya utalii, Dk. Shein alieleza kuwa ndani ya miaka mitatu iliyopita idadi ya watalii imeongezeka kwa kiasi kikubwa huku akieleza mikakati ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar katika kuongeza idadi ya watalii hadi kufikia mwaka 2016.
Dk. Shein alisema kuwa miongoni mwa juhudi zinzochukuliwa hivi sasa ni pamoja na ujenzi wa Jengo jipya la abiria,njia za kutulia na kurukia ndege pamoja na maegesho ya ndege ambapo pia alimueleza azma ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kukiimarisha kiwanja cha ndege cha Pemba ikiwa ni pamoja na kukiweka taa ili ndege ziweze kuruka na kutua wakati wote.
Akizungumzia suala la usalama kwa watalii, Dk. Shein alisema kuwa Serikali inachukua juhudi za makususdi katika kuhakikisha suala la usalama kwa watalii linafanyiwa kazi kwa kuvishirikisha vikosi vya ulizi na usalama vya Serikali kwa mashirikiano ya pamoja na Polisi jamii hatua ambayo imeendelea kuipa heshima kubwa Zanzibar.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar                

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

Related

OTHER NEWS 510035677337564085

Post a Comment

emo-but-icon

FOLLOW US

.

LISTEN / DOWNLOAD MUSIC HERE:

Total Pageviews

RECENT

Archive

item